Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA) imekuwa ikitoa msaada wa kiufundi na mafunzo kwa wakaguzi wa dawa wa nchi wanachama wa Jumuiya ya Kiuchumi ya nchi za (SADC) ili nchi hizo kwa pamoja ziweze kufikia viwango vya kimataifa katika ukaguzi na mifumo ya udhibiti na ukaguzi wa dawa hivyo kufikia lengo la nchi zote za SADC kudhibiti dawa kwa mifumo iliyosawa katika kuwalinda watumiaji wa dawa na vifaa tiba.
Akizungumza na waandishi wa habari kwenye banda la maonesho la taasisi hiyo kando ya mkutano wa Mawaziri wa Afya na UKIMWI wa nchi za SADC, Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Mamlaka hiyo Bi. Gaudensia Simwanza amesema wakaguzi wa dawa kutoka nchi za SADC, walio wengi wamekuja kujifunza na kupata ujuzi kutoka (TMDA) ili kujua namna mifumo yao inavyoweza kudhibiti, ubora na usalama wa dawa ikiwa ni pamoja na ukaguzi katika nchi zao.
Ameongeza kuwa Tanzania imekuwa ni nchi ya kwanza Afrika kwa mifumo yake kutambuliwa na Shirika la Afya Duniani (WHO) kwa kufikia ngazi ya tatu katika udhibiti, ubora na usalama wa dawa (WHO Maturity Lever III).
Nchi za SADC zinafaidika na Tanzania kwa kufikia viwango hivyo vya kimataifa kwani kwa sasa tayari TMDA inatoa msaada wa kiufundi kwa wataalam mbaimbali na wakaguzi wa nchi za SDAC na kutoa ushauri kwa viwanda vya kuzalisha dawa vinavyojengwa ili kuzalisha dawa zenye viwango, Ubora na Usalama kwa watumiaji wa dawa hizo
“Hii ni hatua ya kujivunia kama nchi kwa kufikia viwango hivyo vya kimataifa kwa sababu hii inawafanya watanzania pia kuwa na uhakika wa viwango vya dawa wanazotumia kwa kuwa zimepitia katika mifumo ya udhibiti na usalama wa ubora wenye uhakika na wa kimataifa”.
Amesema Mkutano huo wa Mawaziri wa Afya wa nchi za SADC utajadili mambo mbalimbali kuhusu masuala ya Afya ukiwemo UKIMWI kwa sababu hizi dawa za kufubaza UKIMWI pia ni muhimu zipitie katika mifumo bora kabisa ya udhibiti wa ubora na usalama ili wakati watumiaji watakapozitumia suala zima la usalama wao liwe la kwanza kuzingatiwa.
“Ndiyo maana na sisi kama Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba tuko hapa ili kujua nini kinajadiliwa ambacho kitafaa kwetu kuchukua hatua na kukifanyia kazi kwa upande wetu” ameongeza Simwanza.
Ameongeza kuwa mkutano uliofanyika mwezi Septemba mwaka huu sambamba na mkutano wa nchi za Jumuiya ya Kiuchumi ya SADC ulikuwa na lengo la kutoa mafunzo kwa wakaguzi kutoka nchi mbalimbali za SADC namna ya kufanya ukaguzi na udhibiti wa dawa katika viwanda vinavyozalisha dawa ili kuwa na dawa zitakazokuwa na ubora na usalama kwa watumiaji.

Comments
Post a Comment
Yes