Na Ahmad Mmow, Lindi.
Tani 37 na kilo 599 za pweza wenye thamani ya shingi 150,396,000 walivuliwa kwa muda wa siku tatu baada ya kufunguliwa mwamba laini katika kijiji cha Songosongo,wilaya ya Kilwa mkoa wa Lindi.
Hayo yameelezwa na mtendaji wa mradi wa usimamizi wa uvuvi katika wilaya za Mtwara, Kilwa na Kibiti wa shirika la kimataifa la usimamizi na uhifadhi wa mazingira duniani( WWF), Thomas Charles alipozungumza na Muungwana Blog mjini Kilwa Masoko leo.
Thomas alisema baada ya kufunguliwa mwamba laini uliofungwa katika eneo la bahari ya Hindi lililopo katika kijiji cha Songosongo, pweza wenye uzito watani 37 na kilo 599 zenye thamani ya shilingi 150,396,000 walivuliwa kuanzia tarehe 29. 9.2019 hadi tarehe 1.10.2019.
" Niuvunaji mkubwa ambao haujawahi kufanyika katika ukanda huu wa Afrika Mashariki. Pweza hao niwengi kulinganishwa na muda uliotumika kuvua," alisema Thomas.
Mtendaji huyo alibainisha kwamba tani 23 kati ya tani hizo 37.599 zilinunuliwa na kampuni ya TANPESCA, ambayo ni mmiliki wa kiwanda cha kusindika samaki kilichopo katika wilaya Mafia, mkoa wa Pwani. Huku tani nyingine zilizosalia zilinunuliwa na kampuni nyingine.
Alitoa wito kwa wavuvi wawe waaminifu kwakutoingia nakuvua kwenye maeneo ambayo wananchi wa maeneo hayo wameamua kuyapumzisha kwa muda maalumu yasifanyike shughuli uvuvi. Huku akiwaasa wananchi kutunza na kuhifadhi raslimali za bahari ili yawe na uvunaji endelevu.
Thomas alisema tangu kuanza mpango wa kufunga( kupumzisha) na kufungua mwamba katika katika eneo hilo ni mara ya nne. Ambapo kiasi cha pweza wanaovuliwa kimekuwa kikipanda.
Maeneo mengine ambayo yanapumzisha miamba ni Somanga,Songomnara na Kivinje katika wilaya ya Kilwa na katika wilaya ya Kibiti ni kijiji cha Pongwe.

Comments
Post a Comment
Yes